YENYE KUBATILISHA UPAKAZAJI WA KHOFU

Wanawazuoni wa fani hii ya fiq-hi (Mafaqihi) wamekongamana na kuwafikiana kwamba kila lenye kutengua na kubatilisha udhu pia hubatilisha upakazaji juu ya khofu.

Kwa nini? Hii ni kwa sababu upakazaji juu ya khofu ni sehemu ya udhu na ni badali ya kuosha miguu. Kwa mantiki hiyo kinachotengua na kubadilisha asli (udhu) hubatilisha pia tanzu/tawi (upakazaji juu ya khofu).

Mbali na hili, huongezeka pia mambo mengine matatu, ambayo ni:-

1. Kuisha/kumalizika muda wa upakazaji ulioruhusiwa kisheria kwa mkazi na msafiri. Muda huo utakapomalizika, mpakazaji anatakiwa kwa mujibu wa sheria azivue khofu zake, kisha atawadhe udhu kamili, hapo ndipo anaweza kuzivaa tena kwa twahara hii mpya na kupata ruhusa ya kupakaza juu yake atakapotawadha tena, pia muda mpya utaanzia hapo.

2. Kupatikana kwa jambo linalowajibisha josho kama vile janaba, hedhi au nifasi. Katika hali hii imempasa na kumlazimu mpakazaji kuzivua khofu, akoge josho lililomuwajibikia, kisha ndipo anaruhusiwa kuzivaa tena ikiwa anaona kuna haja ya kufanya hivyo.

Imepokelewa hadithi na Swafwaan Ibn Assaali – Allah amuwiye radhi – amesema: “Mtume wa Mwenyezi Mungu alikuwa akituamrisha tunapokuwa safarini tupakaze juu ya khofu zetu na wala tusizivue kwa muda wa siku tatu kutokana na kukidhi haja kubwa/ndogo na kulala ila kutokana na janaba (tu)”. Tirmidhiy na Nasaai.

3. Mtu kuzivua khofu zote mbili au mojawapo hata kama ikiwa uvuaji huo ni kwa kutoa sehemu kubwa ya mguu bila ya kuutoa mguu wote. Au kwa kutoboka khofu kiasi cha kuuonyesha mguu. Katika hali zote hizi imempasa mpakazaji kuzivua.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *