Ukweli ni mtu kulieleza jambo kama kilivyo bila yakupunguza au kuzidisha chochote.
Muislamu huwa ni mkweli apendaye kusema ukweli na kujitazamisha na tabia ya ukweli hii ni kwa sababu anatambua ukweli humuongezea katika wema, wema ambao humuongoza (kumpeleka) peponi na pepo ndio lengo kuu la muislamu.
Muislamu hauangalii ukweli kama ni tabia njema anayopaswa kujipamba nayo tu bali huenda mbali zaidi ya hapo. Huuona ukweli kuwa ni miongoni mwa mambo yanayoikamilisha imani na uislamu wake: Mwenyezi Mungu anatuagiza:-
“ENYI MLIOAMINI: MCHENI ALLAH NA KUWENI PAMOJA NA WAKWELI” (9:119)
Ukweli umejengeka juu ya sababu tatu, ambazo ni:-
Akili – akili timamu ndio humfanya mtu anayetambua manufaa ya ukweli na madhara ya uwongo.
Murua – mtu mwenye murua, murua wake haumruhusu na kumuachia kusema uwongo bali humlazimisha ajipambe na tabia ya ukweli
Dini – Dini pia humfinyanga mtu ksema ukweli kwa kuamini kuwa dini inamuamrisha kusema ukweli na inamkataza kusema uwongo.
Ukweli pia ni miongoni mwa sifa njema walizopambika nazo Mitume wa Mwenyezi Mungu. Qur-ani yatuambia:-
“NA MTAJE IDRIS KATIKA KITABU (hiki). BILA SHAKA YEYE ALIKUWA MKWELI SANA NA NABII”. (19:56)
Tabia ya ukweli huzaa matunda mema na mazuri ambayo huvunwa na watu wakweli. Miongoni mwa matunda hayo ni:-
Utulivu wa nafsi – Mwenye kupambika na tabia ya ukweli huwa na utulivu wa nafsi kwa mujibu wa kauli ya Mtume: “Ukweli ni utulivu” – At-tirmidhiy
Baraka katika chumo na ziada ya kheri – Bwana Mtume amesema:
“Wauzianaji(Muuzaji na mnunuzi) wana khiyari (ya kupitisha au kuvunja biashara) muda wa kuwa hawajatengana, wakiwa wakweli na wakabainisha (aibu za kinachouzwa) watabarikiwa katika biashara yao, na wakificha (aibu) na wakasema uongo itafutwa baraka ya biashara yao” Al-bukhaariy
Kufuzu kwa kupata daraja ya mashahidi, hili linathibitishwa na kauli ya Mtume aliposema:
“Mtu atakayemuomba Mwenyezi Mungu kufa shahidi kwa ukweli, Mwenyezi Mungu atamfikisha daraja ya mashahidi hata akifia kitandani”. Muslim
Kuepuka balaa, inasimuliwa kwamba mtu mmoja aliyekuwa anakimbizwa alikimbilia kwa mtu mwema mmoja akamuomba amfiche hasikamatwe.
Yule mtu mwema akamwambia; “Lala hapa”, akamfunika na rundo la makuti.
Wale waliokuwa wanamkimbiza wakapita pale kwa yule mtu mwema wakamuuliza :”Umemuona mtu akipita hapa anakimbia?” Akawajibu:
“Huyo hapo chini ya makuti“. Wale watu wakamuona nawafanyia maskhara wakampuuza wakaenda zao. Yule mtu aliyekuwa akikimbizwa akaokoka kwa bababu ya ukweli wa mtu mwema yule.
Kuchuma mapenzi ya Mola na watu. Mtu mkweli hupendeza mbele ya Mwenyezi Mungu na watu na watu wema humpenda.