Hii ndiyo nguzo ya kwanza ya swala.
Maana ya nia kwa ujumla.
Hili ni kusudio la kutenda jambo/kitu Fulani hali ya kulikutanisha kusudio hilo na kitendo makusudi (kilichokusudiwa)
Maana ya nia katika swala.
Ni katika swala ni kuhudhurisha mwenye kuswali moyoni mwake kuingia ndani ya swala anayotaka kuiswali.
Mahala pa nia ni moyoni na wala haikushurutizwa kuitamka kwa ulimi katika kuithibitisha nia ijapokuwa ni bora zaidi kukitamka kile anachokinuia, kwa mfano atasema anapotaka kuswali swala ya Ishaa.
USWALLIY RBAA RAKAAT FARDWHWAL ISHAAI LILLAAHI TAALA.
Akiwa anamfuata Imam atasema
MAAMUMA
Na iwapo yeye ndiye Imam aseme
IMAAMA
Miongoni mwa dalili zinazothibitisha kwamba nia ni nguzo ya swala ni kauli yake Bwana Mtume Rehema na Amani zimshukie:
“bila ya shaka kusihi kwa matendo yote kumefungamana na nia —” Bukhaariy na Muslim.
Ili nia isihi ni lazima ikutanishwe na “Takbiyratul-Ihraam” – Takbira ya kuhirimia swala.
TANBIHI:
Haitoshi tu ile nia anayotoka nayo mtu nyumbani kwenda msikitini kuswali.
Hii kwa yakini si nia bali ni AZIMIO kwa kuwa bado haijakutanishwa na kitendo chake ambacho ni swala yenyewe ambayo haianzii nyumbani kwake mtu.
Mwenye kuswali inampasa asite kidogo kabla ya kuleta Takbiratul – Ihraam aihudhurishe nia ya swala anayotaka kuiswali kwa kuyatamka moyoni au moyoni na ulimini mfano wa maneno tuliyoyataja hivi punde tu.
Hii ni kwa sababu nia aliyotoka nayo mtu nyumbani kuja msikitini ina kazi nyingine maalum ambayo sio ile ya wajibu wakati wa kuleta Takbiyratul-Ihraam.
Hivyo ndiyo inavyofahamisha hadithi sahihi ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie
“Atakayejitwaharisha nyumbani kwake, kisha akaenda katika nyumba mojawapo miongoni mwa majumba ya Mwenyezi Mungu. Zitakuwa Khatua zake mbili, moja inaporomosha dhambi moja na ile nyingine inainua daraja moja”. Bukhaariy na Muslim.
Hii ndiyo kazi ya nia anayotoka nayo mtu nyumbani kwake kwenda msikitini kuswali .
Nia ya swala inayozingatiwa kisheria ni ile inayokutanishwa na Takbria ya kuhirimia swala.