Sharti za iqaamah ndizo zile zile sharti za adhana, zirejee katika somo la adhana utazikuta. Hakuna sababu wala dharura ya kurudia kuzitaja tena hapa.
SUNA ZA IQAAMAH:
Hizi nazo ni zile zile suna za adhana isipokuwa hapa katika iqaamah kuna ziada kama ifuatavyo:-
MUADHINI KUTAWALIA IQAAMAH:
Ni bora mtu aliyeadhini ndiye akimu swala kwa kufuata suna ya Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Atakayeadhini ndiye atakayekimu”. Lakini akiadhini mtu mmoja na akakimu mwingine itajuzu.
KUJIBU IQAAMAH:
Kumesuniwa kwa mwenye kuisikia iqaamah kusema: “AQAAMAHALLAAHU WA ADAAMAHAA” Abuu Daawoud
KUBADILISHA MAHALA PA ADHANA NA IQAAMAH:
Ni suna iqaamah isiwe mahala pa adhana, yaani mtu akiadhini hapa basi akakimu kule.
Asiadhini na kukimu sehemu hiyo hiyo, usuna huu haulengi kuibatilisha adhana na iqaamah vilivyofanywa mahala pale pale.
Bali unakusudia kueleza ilivyo bora na suna ni vipi. Na iqaamah iwe kwa sauti ya chini zaidi kuliko ile ya adhana.
IDHINI YA IMAMU KATIKA IQAAMAH:
Muadhini hapaswi kukimu swala ila kwa idhini ya imamu, kwani hivyo ndivyo alivyokuwa akifanya Bilali; muadhini wa Mtume.
Katika hadithi ya Ziyaad Ibn Al-Haarith amesema:
“Nikawa ninamwambia Mtume-Rehema na Amani zimshukie-nikimu nikimu?”
Kadhalika amesema Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Muadhini ndiye mwenye haki ya kumiliki adhana na imamu ndiye mwenye kumiliki iqaamah”. Ibn Adiy
MAAMUMA WASIINUKE KABLA YA IMAMU WAO:
Itapokimiwa swala, maamuma wasiinuke mpaka ainuke imamu wao kwanza au awaruhusu kuinuka kabla yake.
Haya yanatokana na kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie:
“Itakapokimiwa swala, msiinuke mpaka mnione mimi (nimeinuka)”. Bukhaariy & Muslim
Maamuma wanatakiwa kuinuka kuswali mara baada ya kumalizika kwa iqaamah, hivi ni iwapo wamo msikitini pamoja na imamu wao.
TANBIHI:
Kunashurutizwa kutokuwepo mwanya mrefu baina ya iqaamah na swala, na mwanya ukirepa (ukirefuka) au likapatikana tendo linalohesabiwa kuwa ni mkata iqaamah.
Tendo hili ni kama vile mtu kula baada ya iqaamah, katika hali na mazingira kama haya kutapasa kuirudia tena iqaamah.
Ni suna imamu kuhirimia swala mara tu baada ya kumalizika kwa iqaamah.
Asiache mwanya mrefu baina ya iqaamah na ihraamu ila kwa kiasi cha kujishughulisha na jambo la suna.
Mithili ya imamu kuwaamrisha maamuma wake kunyoosha safu zao, ageuke kuliani na kushotoni kwake akisema: ISTAWUU RAHIMAKUMULLAAH. Maana: Linganeni sawa, Allah akurehemuni.
Katika suala hili, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akisema kuwaambia maswahaba wake:
“SAWUU SWUFUUFAKUM, FAINNA TAS-WIYATIS-SWAFFI MIN TAMAAMIS-SWALAAH”. Bukhaariy & Muslim.
Haijuzu iqaamah ya mwanamke kwa mwanamume.