Ndugu zanguni Waislamu, jamii yoyote ya wanadamu inahitaji sera na utaratibu maalumu wa malezi ili kupata kizazi na jamii njema itakayoufanya ulimwengu huu kuwa ni kisiwa cha amani. Sera utaratibu huu na malezi ni lazima ujengwe juu ya nguzo tatu zifuatazo:-
1. Nguvu
2. Upendo, na
3. Unyenyekevu.
Tunakusudia nini tunaposema nguvu?
Nguvu zikusudiwazo hapa ni nguvu za mwili, roho na akili, ama mradi wa upendo ni kuiangalia jamii ya kiislamu, kwa jicho la rehema na upole na kuitazama jamii ya wanadamu kwa ujumla mtazamo wa kusaidiana na kufahamiana.
Kwa neno unyenyekevu hatukusudii kingine zaidi ya kuondosha tofauti na matabaka katika jamii ya kiislamu (Umma).
Tajiri asijikweze juu ya fakiri kwa sababu tu ya utajiri wake, wala watu waliobeba dhamana mbalimbali serikalini wasijione kuwa ni bora kuliko wananchi wa kawaida eti kwa sababu tu ya nyadhifa zao.
Kadhalika watu wasijifakharishe na kujivuna kwa nasabu, mavazi, na mali zao, bali kigezo chao cha ubora, heshima na utukufu kiwe ni ucha-Mungu (Taq-wa) tu basi.
Tusome na tuwaidhike
’…..HAKIKA AHISHIMIWAYE SANA MIONGONI MWENU MBELE YA ALLAH NI YULE AMCHAYE ALLAH ZAIDI KATIKA NYINYI…….” (49:13) Bahati kubwa na sudi njema waliyonayo Waislamu ni kuwa na sheria bora na kamilifu kuliko sheria zote zilizobaki kuwepo, zilizopo na zijazo.
Sheria ambayo imehodhi sera/utaratibu huu wa malezi, sera ambayo imewafanya watu wote kuwa ni sawa.
Kigezo na dalili kubwa juu ya hili ni ibada kama vile swala, swaumu n.k. kitu ambacho Uislamu umekifanya kuwa ndio msingi na nguzo yake madhubuti.
Hebu sasa na tupekue na kubahithi kwa pamoja ili tuone ni vipi tunavyoweza kuipata misingi ile mitatu ya malezi katika ibada ya swala.
Tuanze na ule msingi wa kwanza.