Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

VITA VYA JAMAL                        Inaendelea...

Kisha akamteua Qa’aqaa bin Amrou kuwa mjumbe/mpatanishi baina yake na Twalhah na Zubeir na akamwambia: Nenda kawaitie kwenye masikizano na jamaa (umoja wa umma) na waase juu ya hatari kubwa ya faraka/utengano. Halafu tena akamuuliza: Haya hebu niambie, utawafanya nini wale watako kujia kutoka upande wa wawili hao, ambao hawana wasia? Akajibu: Tutakutana nao kwa vile/namna uliyo amrisha. Na wakituletea yale ambayo sisi hatuna rai yako katika kadhia hiyo, tutajitahidi kwa rai yetu na tutazungumza nao kama tunavyo sikia na kuona kuwa inafaa. Akasema Sayyidna Aliy: Wewe ndio mstahiki hasa wa hili. [TAARIKHUT-TWABARIY 03/29, AL-FITNATU WA WAQ’ATUL-JAMAL sah. 145 & AL-KAAMIL 03/122 & AL-MUNTADHWAM 05/75].

Mjumbe wa Amani wa Imamu Aliy; Qa’aqaa akawasili Basrah, akaianza kazi aliyo tumwa kwa kuonana kwanza na mama wa waumini, akamuuliza: Ewe mama wa waumini! Ni lipi lililo kuleta kwenye mji huu? Akajibu: Ewe mwanangu! (Lililo nileta huku) ni kufanya suluhu baina ya watu (Waislamu). Akamwambia: (Ikiwa hilo ndilo lililo kuleta) basi naomba uwaitishe Twalhah na Zubeir ili upate kusikiliza maneno yangu na yao. Akawatumia ujumbe wa wito, nao wakaitika, walipo fika Qa’aqaa akasema: Mimi nimemuuliza mama wa waumini ni lipi lililo mleta huku, akasema amekuja kufanya suluhu baina ya watu. Basi je, na nyinyi mnasemaje (ni lipi lililo kuleteni)? Je, nyinyi mnamfuata mama au mnamkhalifu? Wakajibu: Tunamfuata. Akawaambia: (Ikiwa msemavyo ndivyo) basi hebu nielezeni hiyo njia ya usuluhishi, kwani wallah sisi tukiijua, hapana shaka tutakubali suluhu. Na kama tutaikataa (kwa kuwa si ya haki), haitofaa (kuwa ndio njia ya suluhu). Wakasema: (Njia yenyewe ni kuwakamata na kisha kuwahukumu) wauaji wa Uthman, kwa sababu kuachwa kwa jambo hili (bila ya hatua yoyote stahiki), kutakuwa ni kuacha (kuifuata) Qur-ani. Akawaambia: Nyinyi mmekwisha waua wauaji wa Uthman katika watu wa Basrah. Na nyinyi kabla ya kuwaua watu hao, mlikuwa karibu mno na msimamo (wa haki) kuliko mlivyo leo, mmewaua watu mia sita! Kwa ajili hiyo basi, wakaghadhibika kwa ajili yao watu elfu sita, wakajitenga nanyi na wakajitoa kundini mwenu. Na mkataka (kumuua) Hurquusw bin Zuheir, akahamiwa dhidi yenu na watu elfu sita. Basi lau mngeli waacha, mngeli yaacha mnayo yasema na mngeli wapiga vita na wale walio jitenga nanyi, bila ya shaka mngeli wanusuru na kuwashinda. Basi lile mlilo lichelea na mkalitia nguvu kwalo jambo hili, hilo ni kubwa kuliko hilo nionalo mnalichukia. Na ikiwa nyinyi mtawazuilia na mji huu ukoo wa Mudhwar na Rabeea, watajumuika katika kukupigeni vita na kukutupeni mkono, ili kuwanusuru hao kama walivyo jumuika hawa dhidi ya wadau wa tukio hili kubwa na dhambi kubwa.

Mama wa waumini naye akasema: Je, wewe unasemaje? Akajibu: Mimi ninasema hakika dawa ya jambo hili ni kutulizwa na likitulia watu wataona athari yake. Na iwapo nyinyi mtafunga baia kwetu, hiyo itakuwa ni alama ya kheri, bishara, rehema na kudiriki kisasi. Na ikiwa nyinyi mtakataa ila kulikuza jambo hili na kutumia nguvu, basi hiyo itakuwa ni alama ya shari. Basi hebu ifadhilisheni mno afya mtakayo ruzukiwa na kuweni nyinyi funguo za kheri kama mlivyo kuwa. Na wala msituambalizie kwenye balaa nanyi mkaiingia balaa hiyo, kwa hivyo ikatupiga mweleka sisi na nyinyi pia. Na ninamuapia Allah haya ndiyo maneno niyasemayo mimi na ninakuiteni kwayo. Nami ninachelea kutotimia mpaka Allah aitwae haja yake kwa umma huu, ambao zimekuwa chache starehe zake na umefikwa na mabalaa yaliyo ufika. Kwani hakika jambo hili lililo tokea, si kama kadhia ya mtu kumuua mwenzake, wala kundi la watu kumuua mtu mmoja na wala kabila zima kumuua mtu mmoja.

Wakasema (hadhira): Kwa yakini umesibu (umepatia/umesema ndivyo khasa) na umetenda wema. Iwapo Aliy atarejea naye akiwa na rai/maoni kama ya kwako, suala hili litatengenea.

Bwana Qa’aqaa akarejea kwa Imamu Aliy na kumpasha khabari ya yaliyojiri katika utumwa wake. Khabari hiyo ikampendeza na kumfurahisha na kaumu ikakurubia kufanya suluhu. Na ujumbe wa watu wa Basrah ukaja kwa ndugu zao katika watu wa Koufa, ili wapate kuijua rai ya ndugu zao hao (katika kizungumkuti hiki kilicho wakumba Waislamu). Wakawakuta watu wote wa Koufa wamekongamana juu ya suluhu na wala hata kusiwapitikie akilini mwao kupigana na ndugu zao. Basi wakarejea Basrah na wakawaelezea wakaazi wake khabari hii ya kufurahisha. Imamu Aliy akainuka kuwakhutubia Waislamu, akaanza kwa kumuhimidi na kumsifia Allah. Kisha akataja ubaya wa jaahiliya sambamba na saada/wema wa Uislamu na neema ya Allah juu ya umma kwa kuufanya kuwa jamaa (moja) chini ya khalifa baada ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Kisha chini ya khalifa aliye mfuatia (mtangulizi wake), kisha aliye mfuatia huyo. Kisha tena ndipo lilipo tokea tukio hili, lililo letwa kwa umma na watu waitakayo na kuiendea mbio Dunia hii. Watu walio mfanyia hasadi mtu aliye pewa neema na Allah na wakataka kuurejesha Uislamu na mambo nyuma huko yaliko toka. Na Allah ni Mtimizaji wa jambo lake. Ehee, fahamuni ya kwamba mimi ninaingia safarini kesho na kabisa asiingie safarini pamoja nasi yeyote aliye msaidia Uthman kwa lolote katika mambo ya watu. Waacheni masafihi wasaidiane wao kwa wao.

Wasabai (wafuasi wa Abdullah bin Sabai) walipo yasikia maneno yaliyo semwa na Imamu Aliy, wakajuta na wakaona ya kwamba madhara ya suluhu hiyo yatawarudia wao, kwani kama itatimia suluhu hiyo natija yake itakuwa ni wao kuuawa. Kwa kuliona hilo, wakashauriana wafanye nini ili kuizuia suluhu hiyo kufanikiwa. Akasema kiongozi wao aliye mpotevu na pandikizi katika Uislamu: Enyi watu wangu! Hakika utukufu wenu umo katika kuwaparaganya watu. Sikilizeni, kesho watakapo kutana watu, basi nyinyi simikeni (anzisheni) vita na wala msiwape nafasi hata finyu ya kuchunguza/kutafakari kulikoni. Kwa hivyo basi, wale ambao nyinyi mko pamoja nao hawatakuwa na njia ya kujizuia kupigana. Na Allah atamshughulisha Aliy, Zubeir na Twalhah na wote walio na fikra kama zao (za suluhu), wayasahau yote muyachukiayo. Basi wote wakakongamana juu ya rai yake na huku watu wakiwa hawajui lolote linalo endelea.

Kulipo pambazuka, Imamu Aliy akaenda mahala pa maagano na Twalhah na Zubeir wakamuendea, majeshi mawili hayo yakakutana nje ya mji wa Basrah. Imamu Aliy akaulizwa na baadhi ya watu wake kuhusiana na nini cha kufanya. Akajibu: Kufanya suluhu na kuzima kichochea fitina, huenda Allah akalikusanya jambo la umma huu na kuuepusha na vita. Akauliza: Na kama wakito liitika hilo? Akajibu: Tutawaacha muda wa kuwa na wao watatuacha. Akauliza (tena): Na kama hawakutuacha? Akajibu: Tutajilinda/tutajitetea. Akauliza: Je, wanayo wao haki katika kadhia hii kama ule wajibu walio nao? Akajibu: Naam (wanayo). Akainukiwa na mtu mwingine, akauliza: Je, unaona watu hawa wanayo hoja katika damu hii (ya Sayyidna Uthman), ikiwa wamemkusudia Allah katika hilo? Akajibu: Naam (wanayo hoja). Akazidi kuuliza: Je, wewe unaona kuwa unayo haki ya kuakhirisha kisasi? Akajibu: Naam (ninayo). Akaendelea kuuliza: Basi je, hali yetu na hali yao itakuwaje kesho iwapo tutaonjwa (na Allah kuingia vitani)? Akajibu: Hakika mimi ninatarajia kutouawa miongoni mwetu wala miongoni mwao yeyote aliye utakasa moyo wake kwa ajili ya Allah, ila Allah atamuingiza peponi. Kisha akasema: “Enyi watu! Wamilikisheni watu hawa mikono na ndimi zenu, wasije wakatutangulia, kwani mkhasimiwa wa kesho ni yule aliye khasimiwa leo”.

Halafu tena Imamu Aliy-Allah amuwiye radhi-akawatumia mjumbe Twalhah na Zubeir awaambie ya kwamba: Ikiwa nyinyi mngali bado na fikra mlizo kuwa nazo wakati mnaachana na Qa’aqaa, basi jizuieni (bakieni huko huko) mpaka tuje tupige kambi na tulikague suala hili. Wakaitika.

Kisha akatoka Zubeir baina ya majeshi mawili yale akiwa amempanda farasi wake, Imamu Aliy akaambiwa: Zubeir huyoo yuwaja! Akasema Imamu: Ama hakika yeye ni mpapia mno wa watu wawili hao kukumbuka, pindi anapo tajiwa Allah. Na Twalhah naye akatoka pia, Imamu Aliy naye akatoka kwenda kukutana nao mpaka zikakabiliana shingo za wanyama wao. Imamu Aliy akawaambia: Naapa, hakika nyinyi mmekwisha andaa silaha na watu (askari wapiganaji). Ikiwa nyinyi mmekwisha andaa udhuru wa kukuokoeni mbele ya Allah, basi mcheni Allah (muogopeni) na wala msiwe kama yule mwanamke anaye uzongoa uzi wake baada ya kwisha usokota ukawa mgumu. Je, mimi sikuwa ndugu yenu katika dini yenu, mkiharimisha kumwagwa damu yangu nami nikiharimisha damu zenu? Basi je, kuna tukio lililo tokea ambalo limekuhalalishieni nyinyi kumwaga damu yangu? Twalhah akasema: Wewe uliwakusanya watu dhidi ya Uthman (wakamuua). Imamu Aliy akawalaani wauaji wa Sayyidna Uthman, halafu akasema: Hivi wewe haukula baia kwangu? Akajibu: Nilikubai na ilhali kukiwa na upanga shingoni mwangu. Kisha Imamu Aliy akamkumbusha Zubeir mambo mengi ili kuulainisha kwayo moyo wake, akamwambia: Unaikumbuka ile siku uliyo pita ukiwa pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa Baniy Ghaanim. Mtume akaniangalia kisha akacheka nami nikamchekea. Wewe ukamwambia: Mwana wa Abu Twaalib haachi tu fakhari yake! Mtume wa Allah akakuambia: “Si mwenye kujifakharisha, kabisa kwa yakini wewe utampiga vita na ilhali ukiwa unamdhulumu”. [TWABARAANIY katika TAARIKH yake 03/37]

Taathira ya maneno ya Amirul-Muuminina; Sayyidna Aliy-Allah amuwiye radhi-ikawa ni kurejea kwa Zubeir ilhali akiapa ya kwamba yeye hatapigana vita na Aliy. Na khususan pale alipo jua ya kwamba Ammaar bin Yaasir yu pamoja na Aliy na ilhali Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikwisha mwambia: “Utauliwa na kikundi kilicho asi”. Bukhaariy [447] & Muslim [2915, 2916]-Allah awarehemu.

Kama kwamba yeye amekwisha hisi ya kwamba yeye amekosea katika Ijitihadi yake, kwa kuwa yeye anafanya amali kwa ajili ya Allah, huwa karibu mno kurejea kwenye haki na kuongokea kwenye swawaabu (ilivyo ndivyo/sawa) huwa ni kwepesi mno. Basi kila mmoja katika wao akarejea kwa watu wake na wote wakiwa hawana shaka na suluhu. Na wakalala usiku wa shwari kwa sababu ya natija ambayo wanakaribia kuifikia.


 


 | Tuandikie |