|
ADABU/TARATIBU NA SUNNA ZA SWAUMU NDANI YA RAMADHANI
Ndugu Muislamu uliye wafikiwa na Allah kuingia ndani ya
ibada hii tukufu ya swaumu ya mwezi wa Ramadhani, leo tena kwa auni
yake Allah Ataadhamiaye tunakutana katika muendelezo wa makala zetu
maalumu za Mimbari ya Ramadhani. Mimbarini kwetu leo tutazungumzia
Adabu na Sunna za swaumu ya Ramadhani. Wewe kama mfungaji unapaswa
kuyajua na kuyafahamu mambo yanayo fungamana na swaumu, ili kupitia
mambo hayo swaumu yako iweze kufanikiwa na upate kuhodhi ujira adhimu
walio ahidiwa wafungaji.
Ewe ndugu Muislamu!
Fahamu ya kwamba ibada ya swaumu inazo adabu/taratibu
ambazo muislamu amesuniwa kujipamba nazo katika kipindi chote cha
kuitekeleza ibada hii ya swaumu. Katika jumla ya adabu na sunna hizo
ni kama zifuatavyo:
KULA DAKU:
Kula daku ewe ndugu muislamu, kwani huko kula daku ni
katika jumla ya taratibu na sunna za swaumu zilizo fundishwa na
kutekelezwa na mwenyewe Mtume wa Allah. Na pia kula daku ni agizo la
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kupitia kauli yake: “Kuleni
daku, kwani hakika imo ndani ya daku baraka”. Bukhaariy &
Muslim-Allah awarehemu.
Na pia amesema Bwana Mtume: “Kipambanuzi baina ya
swaumu yetu na swaumu ya watu wa kitabu, ni kula daku”.
Muslimu-Allah amrehemu.
Na bora ya chakula cha daku ni tende, kwani imekuja
katika hadithi ya Abu Huraira-Allah amuwiye radhi-ya kwamba Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Bora ya daku la
muumini ni tende”. Abu Daawoud-Allah amrehemu.
Na kadhaalika amesema: “Hakika Allah na Malaika
wake wanawaswalia walaji daku”. Ibn Hibbaan.
Zitoshe nukuu hizi katika kukuonyesha umuhimu wa kula
daku na kukuhimiza juu ya hilo. Basi na jitahidi ewe mfungaji kula
daku ijapo kuwa kwa kunywa funda ya maji au kwa kula kokwa ya tende,
kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Kula daku
ni baraka, kwa hivyo msikuache wala kwa mmoja wenu kunywa funda moja
la maji, kwani hakika Allah na Malaika wake wanawaswalia walaji wa
daku”. Ahmad-Allah amrehemu.
Kuchelewesha kula daku:
Ndugu mfungaji!
Fahamu ya kwamba katika jumla ya Sunna za swaumu ni
kuchelewesha kula daku mpaka karibu ya kuingia kwa Alfajiri. Kufanya
hivyo hakupungui kuwa ni kumfuata Mtume wako-Rehema na Amani
zimshukie-kwani imepokewa katika hadithi ya Anas-Allah amuwiye radhi:
“Ya kwamba Mtume-Rehema na Amani zimshukie-na Zaid bin Thaabit
walikula daku, walipo maliza kula daku lao, Mtume aliinuka kwenda
kuswali, akaswali. Tukamuuliza Anas kulikuwepo na muda gani baina ya
kumaliza kwao kula daku na kuingia kwao kwenye swala. Akajibu kiasi
cha muda wa mtu kusoma aya khamsini”. Bukhaariy-Allah amrehemu.
Ndugu mfungaji! Katika kuitekeleza kwako Sunna hii,
tahadhari kula, kunywa au kufanya lolote katika yanayo funguza swaumu
baada ya kuchomoza/kuingia kwa alfajiri, kwani huo ndio mwanzo wa
swaumu.
Kuharakia kufuturu:
Ndugu mfungaji!
Ni Sunna kwako kuharakia kufuturu mara tu baada ya
kuthibitika kuchwa/kuzama kwa jua, kwani huo ndio mwisho wa swaumu.
Sunna hii imethibiti kupitia kauli ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie: “Watu hawataacha kuwa katika kheri muda wa kuharakia
kufuturu”. Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
Na ni Sunna mfungaji kufuturu kabla ya kuswali swala ya
Maghribi kama ambavyo ni Sunna kufuturu kwa kula tende na akitopata
hizo tende basi japo kwa kunywa funda za maji. Na akivikosa vyote
hivyo, basi na afuturu kwa kula chakula au kinywaji chochote halali
alicho kipata. Hivyo ndivyo alivyo fanya mbora wa wafungaji wote;
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Anas-Allah amuwiye
radhi-amesema: “Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa
akifuturu kwa kula tende mbichi na akizikosa basi kwa tende kavu,
kabla ya kuswali. Na akitozipata, basi hupiga funda za maji”. Ahmad
& Abu Daawoud-Allah amrehemu.
Kuomba sana dua:
Ndugu muislamu!
Fahamu ya kwamba dua ya mfungaji lillaah hairejeshwi
patupu, basi usiipoteze fursa hii adimu na adhimu ambamo ndani yake
dua za wafungaji haziruki patupu. Muombe Allah ewe mfungaji, kwa
uyatakayo miongoni mwa kheri na neema za Dunia na Akhera. Na muombe
Allah ndani ya kipindi chote cha ufungaji mpaka wakati wa kufuturu.
Imepokewa kutoka kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Dua
tatu hazirejeshwi patupu; dua ya mzazi kwa mwanawe, dua ya mfungaji
na dua ya msafiri”. Al-Baihaqiy-Allah amrehemu.
Na ni Sunna kwa mfungaji anapo futuru kuomba kwa dua
aliyo kuwa akiiomba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie.
Imepokewa kutoka kwa Ibn Umar-Allah amuwiye radhi: “Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa anapo futuru husema: DHAHABA
DHWAMAU WAB TALLATIL-URUUQ WA THABATAL-AJRU, INSHAALLAH – kiu
kimeondoka, mishipa imelowana na ujira umethibiti pindipo atakapo
Allah”. Abu Daawoud-Allah amrehemu.
Ndugu mfungaji! Ukiwafikiwa kuyatekeleza mambo haya
tuliyo yataja, hiyo itakuwa ni kheri kubwa kwako uliyo wepesishiwa na
Allah, basi yapapie kwa maslahi na manufaa yako mwenyewe.
|