Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

MAJADILIANO NA WATU WA KITABU   Inaendelea...

Ama wito wa tatu uliomo ndani ya aya hizi, ni kauli ya Allah Atukukiaye: “ENYI WATU WA KITABU! MBONA MNAZIKATAA ISHARA (aya) ZA ALLAH ILHALI NYINYI MNASHUHUDIA?”

Yaani: Kwa nini mnazikataa aya za Allah Ataadhamiaye ambazo mnazo somewa na Mtume wake Muhammad-Rehema na Amani zimshukie-na ilhali nyinyi mnaujua ukweli na usahihi wake kwa ujuzi wa yakini, kama ujuzi wa kushuhudia na kuona kwa macho. Na ilhali pia nyinyi mnajua ya kwamba yeye Muhammad ni mtume kweli kama mnavyo wajua watoto wenu, kuwa ni damu zenu.

Na ulizo lililomo ndani ya kauli yake Allah Ataadhamiaye: “MBONA MNAZIKATAA”, linabeba dhima ya dhana nzima ya kuwaumbua na kuistaajabu hali yao na ukanushi walio nao wa kuzikataa aya za Allah pamoja na kuujua ukweli wake.

Na imo ndani ya wito huu ishara inayo onyesha ya kwamba elimu/ujuzi walio pewa, ulikuwa unawataka na kuwapelekea wao kuharakia kuamini na sio kuzikufuru aya za Allah. Aya ambazo zinazo fahamisha juu ya ukweli wake na zimo humo hoja na miujiza aliyo waletea wao Mtume-Rehema na Amani zimshukie.

Kisha Allah-utakati wa mawi ni wake-akawaelekezea wito wa nne, akawakataza humo kuchanganya baina ya haki na batili na kuificha haki, baada ya kuwa alikwisha wakataza kuzikanusha aya, akasema: “ENYI WATU WA KITABU! MBONA KWELI MNAIVISHA UWONGO, NA KWELI MNAIFICHA NA ILHALI MNAJUA?”

Yaani: Enyi watu wa kitabu! Kwa nini mnaichanganya haki iliyo wazi ambayo imetamkwa na vitabu vya mbinguni na akili zilizo salimika. Mnaichanganya haki hiyo na batili mnayo izua nyinyi wenyewe ili kuyaridhisha matamanio yenu?

Na katika kukaririwa kwa wito na herufi ulizi, imo ziada ya kuwaumbua na kuikanusha itikadi na msimamo walio nao na kuidunisha hali yao. Hivyo ni kwa kuwa wao wamekusanya aina mbaya kabisa ya mambo mabaya ambayo la mbele na kubwa lao, ni kule kukanusha na kuzikataa kwao aya za Allah. Na kuchanganya kwao haki na batili na kuificha haki kwa yule aitakaye.

Na walinganiaji (wahubiri) wa upotevu, wanazo njia mbili wanazo zitumia katika kuwapotosha watu;

Ya kwanza: Njia ya kuichanganya haki na batili, kiasi cha kutokujulikana haki ni ipi na batili ni ipi. Na njia hii ndio inayo ashiriwa na kauli yake Ataadhamiaye: “MBONA KWELI MNAIVISHA UWONGO”.

Ya pili: Njia ya kuikataa/kuipinga haki na kuificha ili isiweze kudhihiri na njia hii ndio inayo ashiriwa na kauli yake Ataadhamiaye: “NA KWELI MNAIFICHA”.

Watu wa kitabu walizitumia njia mbili hizi zote, katika kuwakengeusha watu na dini ya Uislamu. Kwani baadhi yao walikuwa wakiziawilisha (wakizifasiri) nukuu (nassi) za vitabu vyao zinazo fahamisha juu ya ukweli wa Mtume-Rehema na Amani zimshukie-tafsiri potofu ambayo huichanganya haki na batili. Wanafanya hivyo ili kuwatia fikra watu kwamba Muhammad si ndiye mtume aliye kuwa akingojewa kama alivyo tabiriwa ndani ya Taurati na Injili. Na wengine walikuwa wakitia shubuha kwenye haki, ili wapate kuwatumbukiza madhaifu wa imani katika uhemewa na uzingazinga. Na wengine walikuwa wakificha au kuondosha nassi (nukuu za maneno ya Allah zilizomo katika vitabu vya mbinguni), zinazo fahamisha ukweli wa Mtume-Rehema na Amani zimshukie-au zile zisizo wafikiana na matashi/maslahi yao.

Na kauli yake: “NA ILHALI MNAJUA”, hii ni sentensi ya hali. Yaani: Na ilhali nyinyi mnajua ya kwamba mnacho kificha na mnacho watatiza watu, ndicho haki na kweli. Au na ilhali nyinyi ni katika watu wenye ujuzi na elimu ya vitabu vilivvyo tangulia, na wala hainasibu mtu aliye hivyo kuificha haki na kuichanganya na batili. Na kijapo kuwa kitendo hicho (cha kuficha haki), huhesabiwa kuwa katika jumla ya madhambi makubwa hata kama kosa hilo limetendwa na mtu wa kawaida (asiye mwanachuoni). Basi bila ya shaka kitendo hicho hicho, pale kitakapo fanywa na mwanachuoni mweledi, mwenye uwezo wa kupambanua baina ya haki na batili, huwa ni kibaya mno na ufisadi wake huwa ni mkubwa mno na hatima yake huwa ni ukorofi mkubwa sana.

Ndugu msomaji wetu-Allah akurehemu-kutokana na maelezo yote yaliyo tangulia, itakubainikia namna ambavyo Qur-ani Tukufu ilivyo tusimulia namna mbali mbali za shubuhaati za watu wa kitabu. Na kuwarudi kwa namna inayo batilisha shubuha hizo, kwa kutumia mantiki sahihi na kwa majadiliano salama, yanayo zikinaisha akili. Na yanayo wazidishia watu wa haki ithibati zaidi juu ya ithibati yao na imani zaidi juu ya imani yao waliyo nayo.

Ndugu msomaji mwema-Allah akurehemu-hii ni mifano teule katika jumla ya mazungumzo/majadiliano, yaliyo jiri pamoja na watu wa kitabu, kama yalivyo nukuliwa na Qur-ani Tukufu.



  

 | Tuandikie |