|
SOMO LA NNE
WASIA WA UANGALIZI.
Fasiri ya wasia wa uangalizi:
Wasia wa ungalizi/usimamizi ni tafsiri ya neno la Kiarabu “Iiswaau”,
neno ambalo limeteuliwa na Mafaqihi (Wataalamu wa fani ya Fiq-hi)
kuwakilisha/kuelezea dhana nzima ya mtu: Kumuusia mtu aliye na imani
naye, kabla ya kufa kwake, kuwaangalia/kuwasimamia watoto wake,
kuteleza wasia wake, kulipa madeni yake, kurejesha amana za watu
zilizoko kwake na mfano wa hayo, baada ya kufa kwake.
Fasiri ya wasii (msimamizi wa mali/haki/wasia):
Kutokana na maelezo yaliyo tangulia, inabainika maana ya
wasii, ya kwamba yeye ni yule mtu ambaye anaye pewa majukumu ya
kusimamia masuala ya watoto (wa marehemu). Kurejesha amana na kulipa
madeni kwa niaba ya marehemu.
Hukumu ya wasia wa uangalizi:
Lililo asili katika wasia wa uangalizi, ni kwamba huo
umesuniwa, lakini unaweza kuingiwa na mambo yatakayo ufanya kuwa
wajibu.
Imamu Al-Adhra’iy-Allah amrehemu-amesema: “Inadhihiri ya kwamba
ni wajibu kwa akina baba kuusia katika masuala ya watoto, pale
itakapo kuwa hawana babu mstahiki wa utawala. Kumpa wasia huo mtu
muaminifu, mwenye kuheshimika, atakapo mpata. Na akawa na dhana yenye
nguvu ya kwamba yeye akiacha wasia, mali yake itatawaliwa na mtu
mwenye khiana, yaani kadhi au mwenginewe katika watu madhaalimu.
Kwani kumemuwajibikia kuihifadhi mali ya watoto wake, isipotee”.
Na amesema Imamu Al-Baajuuriy-Allah amrehemu: “Wasia wa uangalizi
ulio tajwa ni Sunna, ila katika kukidhi (kulipa) haki aliyo shindwa
(kuikidhi) hivi sasa (katika uhai wake) na ambayo haina mashahidi.
Basi hakika wakati huo wasia wa uangalizi unakuwa ni wajibu, kwa
sababu kuacha kuusia kunapelekea kupotea kwa haki hiyo”.
Kutokana na maelezo yaliyo tangulia, inabainika ya kwamba kuusia
uangalizi/usimamizi ni wajibu pale itakapo kuwa mwenye kuusia anazo
haki zake kwa watu (anadai) au watu wanazo haki zao kwake (anadaiwa).
Ambazo dhana yake kubwa ni kwamba haki hizo zitapotea kama hakuusia
suala la kuzifichua na kuiweka wazi kadhia yake kwa mtu atakaye
chukua mahala pake.
Na hali kadhaalika itakapo chelewa (ogopewa) watoto wadogo kupotea au
kupata madhara, hakika ni wajibu kwa baba yao kutoa wasia kwa mtu
anaye muamini, ili apate kuangalia/kusimamia mambo yao na achunge
maslahi yao.
Ama iwapo hakuna lolote katika hayo yaliyo tajwa, hakika kuusia
uangalizi/usimamizi linabakia kuwa ni suala la Sunna na kitendo
chenye kupendelewa na Sharia.
Hekima/Falsafa ya kuwekwa kwa Sharia ya wasia wa
uangalizi/usimamiaji:
Hekima/falsafa ya kufanya wasia wa uangalizi/usimamizi kuwa
ni jambo la kisharia, ni ule uhitajiwa wake na jamii na kutekelezeka
kwa maslahi ya watu kupitia wasia huo.
Inawezekana mtu akawa katika hali ya kuchungulia kaburi (karibu ya
kufa) na yakawa yapo baina yake na jamii inayo mzunguka, mahusiano ya
kimaada. Kama vile amana zake zilizoko kwa watu au viazimwa vyake
vilivyoko kwao au viazimwa vyao vilivyoko kwake. Na wakati mwingine
huenda akawa na madeni yanayo muwia, akahitajia mtu atakaye simamia
ulipaji wa madeni hayo kwa niaba yake, baada ya kufa kwake. Na
inaweza kutokezea akawa na watoto wasio jiweza, hawana uwezo wa
kuendesha shughuli za mali iliyo achwa na marehemu mzee wao. Kwa
ajili/sababu hiyo basi, maslahi ya watoto hao yakahukumia/yakapelekea
kuwekwa mtu mwenye ujuzi katika shughuli hizo, ili apate kuyasimamia
yote hayo. Ni kwa sababu ya kuyaangalia/kuyazingatia yote hayo, ndipo
Uislamu ukaufanya wasia wa uangalizi/usimamizi, kuwa ni jambo la
kisharia na ukalihimiza na kuliraghibisha (kulipendezeshea nyoyo).
Shartia za Wasia:
Tumesha sema kwamba wasii ni yule mtu anaye pewa majukumu ya
uangalizi/usimamizi baada ya kufariki Dunia kwa mwenye kuusia (muweka
msimamizi). Na ili huyu wasii aweze kuyatekeleza majukumu aliyo pewa
kwa namna bora kabisa, hapana budi zipatikane kwake sharti zifuatazo:
Awe ni mtu mkalafu; yaani awe baleghe (aliye fikia umri wa
utu-uzima) na mwenye akili timamu. Kwani asiye baleghe, mwenye
akili timamu anastahiki kupata wa kutawalia mambo yake na
kuyasimamia masuala yake, basi inawezekanaje kukaswihi kumpa
utawala, ili atawalie mambo ya mwingine?!
Awe muungwana (mtu huru), kwa kuwa mtumwa hana usarifu katika mali
ya baba yake. Kwa ajili/sababu hiyo basi, hafai kuwa wasii anaye
sarifu (panga/dhibiti utumizi, au ustawishaji) katika mali ya mtu
mwingine hata kama atapewa idhini na bwana mmiliki wake.
Awe muislamu na sharti hili ni katika utawalia wa muislamu. Kwa
muktadha wa sharti hili basi, hakuswihi kumpa kafiri wasia wa
uangalizi/usimamizi, ili ayatawalie mambo ya Waislamu, kwani yeye
ni mtuhumiwa, na Allah hakumpa utawala juu yao (hao Waislamu).
Allah Ataadhamiaye anasema: “...WALA ALLAH HATAWAPA MAKAFIRI NJIA
YA KUWASHINDA WAUMINI”. [04:141]
Na amesema-utakati wa mawi ni wake: “ENYI MLIO AMINI! MSIWAFANYE
WASIRI WENU WATU WASIO KUWA KATIKA NYINYI, HAWATAACHA KUKUFANYIENI
UBAYA...” [03:118]
Wasiri wenu: Marafiki wanao ingia katika mambo yenu na mkawa mkiwapa
siri zenu. Hao hawataacha kuyafisidi mambo yenu.
Lakini unaswihi wasia wa uangalizi/usimamizi wa dhimiyu kwa dhimiyu
na kadhaalika dhimiyu kwa muislamu.
Awe muadilifu, asiye jizamisha katika madhambi makubwa wala
kuendelea kuyashikilia madhambi madogo. Na unatosha kwake uadilifu
wa nje; yaani dhaahiri ya hali yake iwe hivyo. Kwa uzingatiaji wa
sharti hili basi, hakuswihi kumuusia uangalizi/usimamizi mtu
fasiki, kwa kuwa wasia ni utawala na uaminiwa, na mtu fasiki sio
muaminiwa.
Awe ni mstahiki wa usarifu (upangaji/udhibiti wa
utumizi/ustawishaji) wa kilicho usiwa (kusimamiwa/kuangaliwa) na
awe na uwezo juu ya hilo. Kwa mujibu wa sharti hili basi, hakuswihi
kumpa wasia wa usimamizi/uangalizi mtu safihi, mgonjwa, mkongwe,
mwenye matatizo ya akili na aliye msahaulifu. Kwa kuwa hakuna
maslahi kumpa utawala mtu ambaye hali yake ndio hiyo.
Hivi ndivyo ilivyo, na kutokana na sharti za wasii zilizo tajwa,
inapatikana faida ya kwamba kunajuzu kumpa wasia wa
uangalizi/usimamizi:
Kipofu, kwa kuwa anaweza kuwakilisha katika masuala ambayo hawezi
kuyajua yeye mwenyewe.
Mwanamke, kwani yeye anafaa kwa kazi ya usarifu.
Sayyidna Umar bin Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi-wakati wa kufa
kwake alimpa wasia wa uangalizi/usimamizi binti yake Hafsah-Allah
amuwiye radhi.
Abu Daawoud [2789]-Allah amrehemu.
Bali yeye huyo mwanamke ndiye aula (bora zaidi) kuliko wenginewe
katika kupewa wasia wa uangalizi/usimamizi, pale zitakapo kusanyika
kwake sharti za wasii, kwa sababu ya huruma yake nyingi aliyo nayo
kwa watoto wake kuliko yeyote asiye yeye.
Hukumu zinazo fungamana na wasii na wasia wa uangalizi/usimamizi:
Kuna mjumuiko wa hukumu nyingi zinazo fungamana na wasii na
wasia wa uangalizi/usimamizi, tunazitaja kwa ufupi kama ifuatavyo:
Hakumuelei (hakumjuzii) wasii kumpa mtu mwingine wasia huo wa
uangalizi/usimamizi. Kwa sababu mwenye kuusia (muweka msimamizi)
alimchagua yeye na hakuuridhia usarifu wa mtu mwingine. Hayo ni
iwapo mwenye kuusia aliuacha huru wasia, bila ya kuufunga na sharti
au alieleza wazi kutokuwakilisha. Ama atakapo mpa idhini ya kufanya
hivyo, basi hakika yeye hazuiwi kufanya hivyo.
Kunajuzu katika wasia wa uangalizi/usimamizi kuweka muda na
kufungamanisha na kitu/jambo.
Lau muweka wasia atasema: “Nimempa fulani wasia wa
uangalizi/usimamizi mpaka atakapo baleghe mwanangu”, au “mpaka
atakapo kuja kaka yangu”, hilo linajuzu. Na kadhaalika lau atasema:
“Nitakapo kufa, basi nimesha kupa wasia wa uangalizi/usimamizi”,
hakika hilo linajuzu, kwa sababu kuusia uangalizi/usimamizi
kunachukua uwezekano wa umajuhuli na fikra za moyo. Na kwa sababu
wasia wa uangalizi/usimamizi ni kama kutawaza uongozi. Na Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimpa uongozi wa jeshi Zaid bin
Haaritha-Allah amuwiye radhi-katika vita vya Mu’utah na akasema:
Akiuawa Zaid, uongozi ushikwe na Ja’afar na akiuawa Ja’afar, basi
uongozi ni wa Abdullah bin Rawaahah. Bukhaariy [4013]-Allah
amrehemu.
Lau mtu atatoa wasia wa uangalizi/usimamizi kwa watu wawili na
asimpe yeyote kati yao uwezo wa usarifu peke yake bila ya mwenzake,
bali alishurutiza kukusanyika wote wawili katika huo (usarifu), au
aliuacha huru, akasema: “Nimemuusia Zaid na Amrou”. Mmoja wao
hawezi kupwekeka na usarifu peke yake, hivyo ni kwa kuifanyia kazi
ile sharti ya kwanza na kutokana na shaka katika ile sharti ya
pili.
Lakini lau mwenye kuusia (muweka msimamizi) atafumbuliza wakati wa
kuusia kila mmoja wao kuwa peke yake katika usarifu, kama vile
kusema: “Nimemuusia kila mmoja kati yenu”, au “kila mmoja kati
yenu ni wasii”. Kumemjuzia kila mmoja kati yao kusarifu peke yake,
bila ya kuwa na mwenzake, kwa sababu ya kuwepo kwa idhini ya hilo
kutoka kwa mwenye kuusia.
Kifungo (mkataba) cha wasia wa usimamizi/uangalizi, ni kifungo
jaaizi (chenye khiyari) kwa pande zote mbili. Kwa hivyo basi,
kunamuelea wasii (msimamizi/muangalizi) kujiuzulu yeye mwenyewe
(katika uangalizi/usimamizi) wakati wowote anapo taka, kama ulivyo
uwakala, kwani yeye ni muwakilishi wa mwenye kuusia. Lakini
kujiuzulu huko kutaswihi iwapo kama haikuwa wajibu juu yake
kuusimamia/kuutekeleza wasia. Na haikuelekea kwenye dhana yake
kutilifu mali ya mwenye kuusia kwa kutawaliwa mali yao na dhaalimu
miongoni mwa kadhi na mwenginewe. Akichelea lolote katika hayo,
hakumjuzii kujiuzulu yeye mwenyewe na wala kujiuzulu kwake
hakutapita, kwa ajili ya kuchunga maslahi ya mayatima na
kuwaondoshea wao hatari au mali yao.
Kunashurutizwa katika kuusia masuala ya uangalizi wa watoto, awe
huyo mwenye kuusia ni miongoni mwa wale walio na utawala juu yao,
kama vile baba au babu.
Wala hakumjuzii baba kumuweka mtu kuwa wasii juu ya watoto wake na
ilhali babu yao yu hai na anazo sifa za utawala. Kwa kuwa utawalia
wake umethibiti kisharia, basi hakumuelei kuuhamisha utawaka kutoka
kwake, kama ulivyo utawalia wa kuozesha.
Mtoto wa mwenye kuusia atakapo baleghe na akazozana na wasii katika
utumizi wa mali na akadai ya kwamba yeye anafanya ubadhirifu.
Katika hali/mazingira hayo, wasii atasadikiwa kwa yamini yake, kwa
kuwa yeye ni muaminiwa mbele ya sharia.
Lau atazozana nae katika kuikabidhi mali kwake baada ya kubaleghe,
katika hali/mazingira hayo atasadikiwa mtoto kwa yamini yake, na hili
ni kwa mujibu wa eleweko (mafuhumu) ya kauli yake Allah Ataadhamiaye:
“...NA MTAKAPO WAPA MALI YAO WASHUHUDIZIENI...” [04:06] Yaani: Na
mnapo wakabidhi mayatima mali yao, wekeni mashahidi wa kushuhudia
hilo.
|