Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

KUCHAGUA MARAFIKI            ...Inaendelea

Hakika urafiki ni wajibu utegemee na ujengeke juu ya nguvu za imani na matendo matukufu. Na bora ya wanacho kidaimisha watu ni tangamano lao na yatasalia duniani na akhera mawada (mapenzi dhati) yao, wale walio kusudiwa na hadithi: “Atakaye amiliana na watu, asiwadhulumu, akazungumza nao asiwaongopee, na akawaahidi na asiwakhalifie miadi yake. Basi huyu ni katika wale ambao umekamilika murua wao na umedhihiri uadilifu wao na umepasa udugu wao”.

Mahusiano ya kirafiki yatakapo anzishwa kwa ajili ya Allah, basi hayatasalia na kumea ila kwa kumtii Yeye Allah. Na wala hayatakuwa na kuendelea ila kwa marafiki wawili hao kujiepusha na unafiki na ufisadi. Angalia, maasi yatakapo penya na kuingia kwenye silka na mwenendo wa aidha mmoja wao au wote wawili, hapo nyoyo hubadilika na mapenzi hukauka. Imekuja katika hadithi: “Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mkononi mwake, hawakupendana wawili kisha wakafarikiana, ila ni kwa sababu ya dhambi anayo itenda mmoja wao”. Ibn Abi Dunya-Allah amrehemu.

Ni kwa ajili hiyo basi, ndio maswahaba wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakawa wanakufanya kuhusiana haki na kusaidiana katika kutenda kheri/wema. Mawili hayo ndio uzio/wigo unao yahifadhi mawada (mapenzi dhati) yaliyo baina yao, na unawakurubishia kwenye msamaha na radhi za Allah. Imepokewa kutoka kwa Abu Qalaabah, amesema: “Watu wawili walikutana sokoni, mmoja wao akamwambia mwenzake: Njoo tumuombe maghufira Allah katika mahala pa mghafala wa watu, wakafanya hivyo. Mmoja wao akafa, mwenzake akakutana naye usingizini, akasema: Nimejua ya kwamba Allah ametusamehe madhambi yetu jioni ya siku ile tuliyo kutana sokoni”.

Na imepokewa kutoka kwa Anas bin Maalik-Allah amuwiye radhi: Alikuwa Abdullah bin Rawaahah anapo kutana na mtu katika maswahaba wa Mtume wa Allah, husema: Njoo tumuamini (tumdhukuru) Mola wetu kitambo kidogo. Siku moja akamwambia maneno hayo mtu mmoja, mtu yule akaghadhibika. Akaenda kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: Ewe Mtume wa Allah! Kwani humuoni mwana wa Rawaahah, anaichukia (anatoka) imani yako na kwenda kwenye imani ya kitambo kidogo? Mtume akasema: “Allah amrehemu mwana wa Rawaahah, hakika anavipenda vikaazi ambavyo malaika hujifakharisha navyo”. Ahmad & Twabaraaniy-Allah awarehemu.

Na inatakikana marafiki wajuane na kufahamiana ili kuhusiana kwao kuwe juu ya ushahidi na mmoja wao amwambie mwenzake mapenzi na uenzi alio nao juu yake. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Mmoja wenu atakapo mpenda nduguye (muislamu mwenzake), basi na amwambie ya kwamba yeye anampenda”. Ahmad-Allah amrehemu.

Na imepokewa kutoka kwa Anas-Allah amuwiye radhi: Mtu mmoja alikuwa kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akapita mfu fulani. Akasema: (yule aliyeko kwa Mtume): Hakika mimi ninampenda huyo (apitaye). (Mtume) akasema: Je, umemjulisha? Akajibu: Hapana. (Mtume) akasema: Basi mjulishe. Akamuendea na kumwambia: Hakika mimi ninakupenda kwa ajili ya Allah. Akasema (mtu mpendwa yule): Akupende Allah ambaye kwa ajili yake wewe umenipenda mimi”. Abu Daawoud-Allah amrehemu.

Na amesema Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Mtu atakapo funga udugu na mtu, basi na amuulize (huyo nduguye) jina lake, ubini wake (jina la baba yake) na ukoo wake, kwani hilo hupelekea zaidi kwenye mawada”. Tirmidhiy-Allah amrehemu.

Na wala hapana shaka kwamba ufanyaji wa mzaha (utani halali/kweli) na ufikiri wa mambo, una mlango mkubwa katika uasisi wa mahusiano ya urafiki, pamesemwa: “Huenda akawa nduguyo wa dhati/ukweli, yule ambaye hamkuzaliwa na mama mmoja”. Kwani huenda ikatokezea katika mchakato wa maisha, mtu akakutana na ambaye anahisi kuoana naye kitabia na kuvutika naye mno, kama kwamba wamejuana miaka mingi. Na hayo ni usadikisho wa hadithi: “Roho ni majeshi yaliyo tayari, zilizo fahamiana katika hayo (majeshi) huungana pamoja na kuzoeana na zilizo kataana katika hayo hutofautiana”. Bukhaariy-Allah amrehemu.

Lakini hisia hizo ni wajibu zitawaliwe na mamlaka ya imani na nidhamu yake. Madaraka hayo ambayo muumini huwa nayo katika mielekeo yote ya moyo wake, ndio humfanya kumpenda kwa ajili ya Allah yule ambaye hajapata kumuona ana kwa ana, kwa sababu ya umbali wa masafa baina yao au kuishi katika zama mbili tofauti. Na kwa ajili hiyo hiyo, kadhaalika humchukia yule ambaye hajapata kuchanganyika pamoja naye si katika mji au safarini. Yote hayo si kwa ajili ya chochote ila tu ni kwamba yeye anawapenda wema na anawachukia waovu. Na mielekeo ya moyo kwa namna hii takasifu, humnyanyua mdau wake daraja nyingi juu ya cheo chake stahiki. Imepokewa kutoka kwa Abu Dharri-Allah amuwiye radhi: Nilisema: Ewe Mtume wa Allah! Mtu anawapenda watu lakini yeye hawezi kufanya amali wanazo zifanya watu hao. (Mtume) akasema: “Wewe Abu Dharri utakuwa pamoja na uwapendao”. Tirmidhiy-Allah amrehemu.

Na miongoni mwa taratibu za Uislamu katika suala zima la mahusiano ya kirafiki, ni kutembeleana ambako hakubebi lengo lingine lolote zaidi ya kukusudia kupata radhi za Allah kupitia mlango huo wa kupenda kwa ajili yake. Imepokewa kutoka kwa Abu Huraira-Allah amuwiye radhi-kutoka kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Ya kwamba mtu mmoja alimtembelea ndugu yake (wa imani) katika kitongoji fulani. Allah akamletea malaika akiwa njiani (kuelekea huko), alipo mfikia akamuuliza: Unakwenda wapi? Akajibu: Ninakusudia kumzuru ndugu yangu katika kitongoji hiki. (Malaika) akauliza (tena): Je, kuna neema unayo ikusudia (kuipata kutoka kwake)? Akajibu: Hapana, ila tu ni kwamba mimi nimempenda kwa ajili ya Allah Ataadhamiaye. Akasema (yule malaika): Basi hakika mimi ni mjumbe wa Allah kwako, (nimetumwa nikubainishie) ya kwamba Allah amesha kupenda kama ulivyo mpenda kwa ajili yake”. Bukhaariy-Allah amrehemu.

Hakika hatua hizi anazo piga mtu kwenda kumtembelea ndugu yake wa imani, ni ghali mno. Hakika hatua hizo, ni kama zile hatua za mujahidina katika njia ya Allah, zinazo jizolea thawabu maridhawa mno. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Atakaye mkagua mgonjwa au akamtembelea ndugu yake katika Allah, atalinganiwa na mlinganiaji: Umetenda vema na yamekuwa mema matembezi yako na umesha jipotelea nyumba peponi”. Abu Daawoud-Allah amrehemu.

Na amesema: “Hapana mja yeyote anaye enda kumzuru nduguye kwa ajili ya Allah, ila hulinganiwa na mlinganiaji kutoka mbinguni ya kwamba umetenda vema na pepo imekuwa njema kwako. Na zaidi ya hivyo, Allah atasema katika ufalme wa Arshi yake: Mja wangu amefanya ziara kwa ajili yangu na ni juu yangu mimi dhifa yake. Naye hakuridhia thawabu zozote ila pepo”. Muslim-Allah amrehemu.

Muislamu ajapo kuwa anawapendelea watu wote manufaa, lakini yeye anawapendelea mno marafiki zake kupata manufaa. Na huzifurahikia mno kheri wanazo zipata na wala si vibaya akipata ziada akawakumbuka rafiki zake: “...WALA MSISAHAU FADHILA BAINA YENU. HAKIKA ALLAH ANAYAONA MNAYO YATENDA”. [02:237]

Yaani: Na kumbukeni kuwa kheri iko katika kufadhiliana na kufanyiana ihsani. Hayo ndio yanayo pelekea kupendana baina ya watu. Na Allah anazijua vema dhamiri zenu na atakulipeni kwa fadhila mzitendazo.

Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amelipendelea suala la kupeana hadiya (zawadi) baina ya marafiki, akasema: “Peaneni hadiya, kwani hadiya huondosha ghushi na wasiwasi wa moyo”. Tirmidhiy-Allah amrehemu.

Na imepokewa kutoka kwa Bi. Aysha-Allah amuwiye radhi-amesema: “Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akipokea hadiya na akiombea thawabu juu yake”. Al-Bazzaar-Allah amrehemu.

Uislamu; dini na mfumo wa maisha unao randana na umbile la mwanaadamu, umeyafanya mahusiano ya urafiki kuwa ni njia ya kuyarahisisha maisha na kuyapunguza magumu yake: “Mbora wa marafiki mbele ya Allah, ni yule aliye mbora wao kwa rafiki yake. Na mbora wa majirani mbele ya Allah, ni yule aliye mbora wao kwa jirani yake”. Al-Haakim-Allah amrehemu.

Hakika Uislamu umemuhalalishia na kumruhusu mtu kula chakula cha rafiki yake, kama anavyo kula chakula cha wazazi wake, ndugu zake na jamaa zake: “...MKILA KATIKA NYUMBA ZENU, AU NYUMBA ZA BABA ZENU, AU NYUMBA ZA MAMA ZENU, AU NYUMBA ZA KAKA ZENU, AU NYUMBA ZA DADA ZENU...” mpaka alipo sema: “....AU ZA WALIO WASHIKIA FUNGUO ZENU, AU RAFIKI ZENU...”. [24:61]

Wala hilo halina ajabu, kwani kifungo cha mahusiano ya kirafiki, kina thamani kubwa na athari tukufu kiasi cha kuwa madhanio ya uokovu katika dhiki kuu. Hata kama zingeli kuwa dhiki/shida hizo ni uokovu kutokana na adhabu ya Jahannamu. Allah Ataadhamiaye anasema katika wasifu wa hali ya washirikina pale watakapo onja ukali wa adhabu: “WALLAH! KWA YAKINI TULIKUWA KATIKA UPOTOVU ULIO DHAAHIRI. TULIPO KUFANYENI NI SAWA NA MOLA MLEZI WA WALIMWENGU WOTE. NA HAWAKUTUPOTEZA ILA WALE WAKOSEFU. BASI HATUNA WAOMBEZI WALA RAFIKI WA DHATI”. [26:97-101]

Na kwa kuwa mahusiano haya ya kirafiki yanafungamana na haki kubwa/nzito, ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Usisuhubiane ila na muumini na wala asile chakula chako ila mchaMngu”. Abu Daawoud-Allah amrehemu.

 

  



 | Tuandikie |